Potassium Cyanide ni kidonge kigumu mno kutengeneza na kinachoua kwa maumivu makali ndani ya sekunde kumi na tano tu! Pindi kinapokutana na asidi za tumboni hubadilika na kuwa gesi ya Hydrogen Cyanide na kupenya harakaharaka katika mishipa ya damu. Hydrogen Cyanide huzuia oksijeni kuingia katika seli hivyo kufanya damu iwe na oksijeni nyingi zaidi kiasi ambacho hakitaweza kutumiwa tena na mwili. Kidonge hiki kilibebwa na John Murphy katika bastola yake ndogo ya Stinger, na katika bastola yake kubwa ya PSS Vul (‘Val’) kama sumu ya kumuua, ili akitekwa akimeze na kufa ndani ya muda mfupi kuliko kutoboa siri za EAC na siri za Tume ya Dunia ya Kudhibiti Madawa ya Kulevya.
Potassium Cyanide si hatari inapokuwa nje. Ni hatari inapojichanganya na asidi za tumboni ambapo hubadilika na kuwa gesi ya Hydrogen Cyanide. Gesi ya Hydrogen Cyanide ni miongoni mwa sumu hatari zaidi ulimwenguni. Mtu akimeza kidonge cha Cyanide atapata madhara makubwa. Kichwa chake kitamuuma hapohapo na atachanganyikiwa akili. Ngozi yake itakuwa nyekundu, kwa sababu damu yake itakuwa nyekundu zaidi, kutokana na kuzidi kwa oksijeni katika damu.
Mwili hautakuwa na uwezo tena wa kuchukua oksijeni kutoka katika damu ili uitumie. Kwa hiyo damu itazidi kuwa na oksijeni zaidi. Atapumua kwa shida. Mapafu yake yatafanya kazi vizuri lakini mwili wake hautakuwa na uwezo wa kutumia oksijeni yoyote. Hivyo atadhani ana matatizo katika mfumo wake wa kupumua. Atazimia. Yaani, oksijeni haitafika kwenye ubongo. Atapata kifafa na atatapika nyongo. Ubongo wake utashindwa kufanya kazi na atakuwa mahututi ndani ya sekunde kumi! Baada ya hapo moyo wake utasimama kufanya kazi, na atafariki dunia.
Kiuasumu ni dawa ya kupoza nguvu ya sumu. Kila sumu ina kiuasumu chake. Viuasumu vya Cyanide ni Amyl Nitrite, Sodium Nitrite, Cyanokit, na Sodium Thiosulfate. Kazi ya viuasumu hivi ni kuzalisha madini mengi ya chuma mwilini. Madini haya yatapambana na maada za rangi za uhai (‘cytochromes’) kwa ajili ya Cyanide ili Cyanide ing’ang’anie kwenye kiuasumu badala ya kung’ang’ania kwenye vimeng’enya vya seli za mwilini. Kiuasumu kinaposhinda mpambano huo, Cyanide hutolewa nje kwa njia ya mkojo na mwathirika wa Cyanide hupona kabisa. Hata hivyo, Sodium Thiosulfate ndiyo bora zaidi kuliko Amyl Nitrite au Sodium Nitrite na ndiyo bora zaidi kuliko Cyanokit.
Kidonge cha Cyanide huweza kuhifadhiwa mdomoni au kwenye pete ili iwe rahisi kukimeza pale mtu anapokuwa kwenye matatizo, na huweza kuhifadhiwa ndani ya kasha la risasi hivyo kuonekana kama Stinger ina risasi mbili wakati ina moja au Vul ina risasi saba wakati ina sita.
Potassium Cyanide huzuia oksijeni kuingia katika seli hivyo kufanya seli zisipate hewa na kufa, baada ya muda mfupi.
No comments:
Post a Comment