Sunday 1 January 2017

Gari la Vijana wa Tume Walilopewa na Jeshi la Anga la Meksiko FAM

Gari la Vijana wa Tume walilopewa na Jeshi la Anga la Meksiko kwa makubaliano maalumu na Tume ya Dunia ya Kudhibiti Madawa ya Kulevya, Mercedes Benz, lilivyosambaratishwa na kombora la magaidi wa Kolonia Santita katika barabara ya Mexico City ya Gobernador Ignacio Esteva, karibu na Ubalozi wa Urusi, lilipokuwa njiani kuelekea Álvaro Obregón katika makao makuu ya Kolonia Santita ya Kiwanda cha Dongyang Pharmaceuticals. Vijana wa Tume walikuwa na mtoto wa Rais wa Meksiko, Debbie Patrocinio Abrego.

Mkurugenzi wa Usalama wa Tume ya Dunia Christoffer Sortevik aliwaagiza Vijana wa Tume wafuate maelekezo yake watakapokuwa Mexico City. Mojawapo ya maagizo hayo ni kwenda San Ángel, Álvaro Obregón, kupitia Lazaro Cardenas, Pedro Moreno, Paseo de la Reforma, Manuel Avila Camacho katika Baraste Kuu ya Anillo Periférico, Adolfo Lopez Mateos, Barranca del Muerto, Avenida Insurgentes Sur, na Avenida de la Paz; lakini wao wakakaidi agizo hilo na kuchukua njia ya mkato ya kupitia 16 de Septiembre, ili wafike Amargura dakika ishirini kabla ya muda waliopanga kufika huko. Amargura ni barabara iliyoko ndani ya kitongoji cha San Ángel, iliyoko katika wilaya ya Álvaro Obregón, kusini-magharibi mwa Mexico City.

Gari lao aina ya Mercedes Benz lilipofika Gobernador Ignacio Esteva, barabara nyembamba iliyokuwa na mitaro ya maji machafu kwa pembeni na taa za kuongozea magari, karibu na Hospitali ya Mocel na Ubalozi wa Urusi, lilisimamishwa na askari wawili wa barabarani. Vijana wa Tume walikuwa na kibali cha kuvunja sheria cha wiki mbili; lakini bado Mogens, aliyekuwa akiendesha, akasimamisha gari.

Mogens alifungua kioo kumsikiliza askari mmoja kati ya wale wawili; huku Murphy, Yehuda na Radia wakiwa makini kwa lolote lakini Debbie akiwa hashangai sana. Vijana wa Tume walishangaa. Tangu waingie Meksiko walikuwa hawajaona askari wa barabarani hata mmoja. Lakini Debbie akawahakikishia ya kuwa hicho hakikuwa kitu cha kushangaza sana kwa Mexico City.

Murphy alimsihi Mogens waondoke kwani walikuwa na kibali cha serikali cha kuwa juu ya sheria kwa angalau majuma mawili, kilichotolewa pamoja na ‘D-Notice’ ya kuwazuia wahariri wa vyombo vya habari nchi nzima kuchapisha taarifa za Vijana wa Tume katika kipindi chote cha Operation DC, lakini Mogens akabisha na kusema haikuwa busara kutumia ubabe katika nchi ya watu.

Bila kujua Mogens alikuwa amefanya kosa. Alikuwa amefanya kosa kubwa la tatu. La pili lilikuwa kukiuka njia ya Sortevik. La kwanza lilikuwa kudharau ratiba ya tume na Murphy na Mogens kuondoka na Debbie na Lisa katika Baa ya Desierto de Los Leones! Wale hawakuwa askari wa barabarani wa kawaida. Zilikuwa njama hatari za magaidi wa Kolonia Santita waliosambaa kila kona ya Barabara ya Ignacio Esteva, mpaka Hospitali ya Mocel na Ubalozi wa Urusi.

Gari la Vijana wa Tume liliposimama, na Mogens kuongea na askari polisi wa barabarani, kitu cha hatari kilifanyika katika gari lao bila wao wenyewe kujua. Askari mmoja, mwenzake na yule mwingine, alipenya harakaharaka na kupachika kitu katika chasisi ya gari la Vijana wa Tume; halafu akatoka na kuelekea upande wa pili wa barabara, ambako aliingia ndani ya gari na kuondoka.

Dereva wa gari moja la nyuma ya gari la Vijana wa Tume hata hivyo, aliona picha yote lakini akaogopa kusema au kufanya chochote. Alijua walikuwa majambazi, na hakutaka shida. Lakini nafsi ilimsuta. Hakuvumilia kuona alichoona. Hivyo, aliamua kuwapa taarifa Vijana wa Tume; bila majambazi kumwona, kwa sababu hakujua walikokuwa wamejificha.

Baada ya wale askari wawili wa Kolonia Santita kufanya uchunguzi wao wa mwisho katika gari la Vijana wa Tume na magari mengine, waliondoka na kuruhusu magari yaendelee na safari zake. Wakati huohuo gaidi mwingine, pembeni ya barabara, ndani ya gari ndogo nyeusi, alikamata kidhibiti cha kulipulia mabomu akiwa na wasiwasi mno na kuchomoa waya wa mawasiliano. Wakati huo Mogens alikuwa ndiyo kwanza anaondoa gari bila kujua kilichokuwa chini ya gari lao, wala kilichokuwa kikiendelea hata katika magari ya watu wengine.

Gari la nyuma lilivuta mwendo kuwa sawa na gari la Vijana wa Tume. Sambamba kabisa na gari lao, msamaria mwema wa lile gari lingine alishusha kioo na kuwapa ishara ya kufungua kioo. Lakini Mogens akasita. Alidhani ulikuwa mtego. Wote walikuwa makini ghafla na kujiuliza nini kilikuwa kikiendelea! Yule bwana alivyozidi kuwatupia ishara, Radia alimwambia Mogens afungue kioo. Kama ni kushambuliwa wangeshambuliwa tu; kwani gari la Vijana wa Tume lilikuwa na inchi mbili tu za vioo vya kuzuia risasi. Harakaharaka Mogens alishusha kioo na kumsikiliza msamaria, ambaye sasa alikuwa amechomoza kichwa nje kwa wasiwasi mkubwa.

“Bomu chini ya gari yenuu!” msamaria mwema alipiga kelele na kurudisha kioo upesi, halafu akaongeza mwendo na kupotea.

Kelele ya msamaria mwema iliwaachia Vijana wa Tume maswali mengi. Hawakujua kwa nini yule mtu alisema vile na wala hawakujua bomu alilosema lilivyowekwa chini ya gari lao wala muda wenyewe wa kuliweka. Murphy alimshika Debbie, kwa nguvu zake zote, na kufungua mlango.

Yule gaidi wa kidhibitimbali alirekebisha antena halafu akakunja uso. Kwa hasira alibonyeza kitufe cha kulipulia, mambo yakawa mengine kabisa katika gari la Vijana wa Tume.

Ulisikika mlio wa moja kwa moja chini ya gari la Vijana wa Tume, kabla ya Mercedes kulipuka vibaya, vibaya sana na kutawanyisha vyuma kila mahali mithili ya volkano! Kama vitu visivyokuwa na uzito Vijana wa Tume walirushwa juu hali kadhalika, na kuangukia barabarani, kila mtu akianguka vibaya na kulala sehemu yake.

No comments:

Post a Comment

Roho Yako

289. Roho yako inatoka wapi? Ya kwangu inatoka Tanzania. Kwa sababu amani na utulivu ndivyo vitu vya muhimu zaidi katika maisha yangu. ...