Monday 2 January 2017

Panoplia

206. Kutoka nyumbani kwako hadi kazini kwako na kutoka kazini kwako hadi nyumbani kwako, umeepuka wastani wa mitego 10,000 ya Shetani! Kuwa na huruma kwa malaika anayekulinda.

Mungu ana uwezo wa kukuwekea ulinzi kulia na kushoto yaani anayekulinda naye ana mlinzi wake. Lakini wakati mwingine anaacha ufuate kile ambacho moyo wako unataka kwa sababu hataki kukulazimisha ijapokuwa uwezo huo anao. Mungu hakukuumba kuwa roboti. Alikuumba kuwa huru kuchagua mema au mabaya usije ukamlaumu baadaye kwamba ulimchagua yeye kwa sababu hukuwa na uhuru. Msikilize Roho wa Mungu, kabla na katika kila jambo unalofanya.

Ndugu zangu, malaika wanatulinda. Wako katikati ya maadui zetu na sisi. Hatujui ni mara ngapi malaika wameingilia kati kuokoa maisha yetu, kutuepusha na nguvu za Shetani na malaika wake wakorofi. Lakini nina hakika ya kwamba wamefanya hivyo mara nyingi katika mazingira ambapo aghalabu sisi huwa hatuelewi.

Mungu anataka tujifunike kwa ngao yake. Yaani, tuwe na imani iliyokomaa katika Bwana na yeye atatufunika. Maana ya kauli hiyo ni kwamba kila kiungo cha miili yetu kuanzia unyayo hadi kichwa lazima kifunikwe kwa silaha ya Mungu, ambayo Mungu anaiita panoplia. Panoplia haimo katika kamusi ya Kiswahili au Kiingereza, lakini maana yake ni ‘ngao kamili ya Mungu’. Hii si tu silaha ya Mungu. Ni silaha kamili ya Mungu tunayotakiwa kujifunika kwayo.

Sasa litambua hili: ushindi ni lazima kwa sababu Daudi wetu Yesu Kristo ameshamshinda Goliati wao Shetani. Amemshinda ili aishi ndani yetu na anaishi ndani yetu. Lakini hatutaweza kumshinda Shetani na malaika wake mpaka tutambue kuwa wapo na tuamini kuwa Mungu atawashinda kama tutampa nafasi ya kufanya hivyo kwa kuwa watiifu kwake.

Kuwa na huruma kwa malaika anayekulinda ni kujifunika kwa silaha kamili ya Mungu. Ukijifunika kwa panoplia utamrahisishia kazi malaika wako, aliyepewa jukumu na Mwenyezi Mungu kukulinda.

1 comment:

  1. Mungu anataka tuwe na upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, na kiasi katika mambo tunayoyafanya. Lakini sifa hizi hazitapatikana hadi tumtii Mungu kupitia Roho Mtakatifu.

    ReplyDelete

Roho Yako

289. Roho yako inatoka wapi? Ya kwangu inatoka Tanzania. Kwa sababu amani na utulivu ndivyo vitu vya muhimu zaidi katika maisha yangu. ...