Wednesday 7 June 2017

LIJUE SHIRIKA LA MADAWA YA KULEVYA LA KOLONIA SANTITA LILILOANZISHWA MWAKA 1980 KWA KUUNGANISHA MAGENGE MAKUBWA 7 YA MADAWA YA KULEVYA YA AMERIKA, MEKSIKO NA KOLOMBIA, NA MAGENGE MENGINE MADOGOMADOGO ZAIDI YA 90 YA AMERIKA YA KUSINI NA KASKAZINI

Historia kwa ufupi ya Kolonia Santita haikuandikwa mpaka zaidi ya miaka thelathini iliyopita katika Jimbo la Oaxaca nchini Meksiko. Desemba 1980 (miaka mitano na mwezi mmoja baada ya kuanzishwa kwa Tume ya Dunia) El Tigre na viongozi 13, wa mashirika 7 ya madawa ya kulevya ya Americas (Amerika ya Kusini na Kaskazini), waliungana katika Mkutano wa Oaxaca na kuunda La Familia (Familia) – kwa lengo la kujiimarisha kibiashara (ndani ya Americas) na kupanua wigo wa biashara yao mpaka nje ya Hemisifia ya Magharibi.

Kutawala biashara ya madawa ya dunia, La Familia ikabadilika na kuwa La Federación (Shirikisho) iliyosambaa kutoka Meksiko mpaka Australia mpaka India mpaka Afrika ya Kusini – na kuwa na nguvu kuliko Medellín ya Pablo Escobar, na Cali ya Gilberto Orejuela, na mashirika mengine mengi ya kipindi hicho katika Amerika ya Kusini na Kaskazini.

Chini ya utawala wa El Tigre kama kiongozi mkuu msaidizi, La Federación ikafungua matawi makubwa saba dunia nzima – Saldanha, Paris, Mumbai, Moscow, Miami, Bissau na Copenhagen – kwa ajili ya ugaidi, wa kimadawa (‘narcoterrorism’), na usambazaji wa madawa duniani kote kwa niaba ya Federación.

Oktoba 1983, hata hivyo, Tume ya Dunia ilipoanza rasmi kumtafuta El Tigre na baadhi ya makamanda wake, La Federación ilisambaratika. Jeshi la Anga la Meksiko (FAM) na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (PGR) vilimuua Kiongozi Mkuu wa Federación (Carlos Pulecio Alcántara) na kuwafunga makamanda wawili wa juu wa muungano wa shirika hilo katika gereza la Mexico City, Reclusorio Preventivo Oriente, alikowahi kufungwa El Tigre na kutoroka katika miaka ya sabini – hivyo kuathiri (kwa kiasi kikubwa) uongozi na biashara ya Federación, hasa ya kokeini (na heroini) duniani kote.

Kurudisha imani ya wateja (na kutambulisha eksitasi na ‘hielo‘ katika soko la dunia la Federación – na kujipanga upya) La Federación ikabadilika na kuwa jina la sasa la La Colonia Santita Cartel (CS-14), Shirika la Madawa ya Kulevya la Kolonia Santita (KS-14), Septemba 1985 katika Mkutano wa Kolombia.

El Tigre na wenzake wanne: Ignacio Leonardo de la Fuente, Raymundo Escoto Martinez, José Alberto Araújo na Panceano Nieto (viongozi waanzilishi wa La Familia; waliokuwa wakitafutwa na Tume ya Dunia na Jeshi la Meksiko sawa na El Tigre na Alcántara) hawakuhudhuria Mkutano wa Kolombia. ‘Jefe de Jefes’ (Bosi wa Mabosi) El Tigre, na wenzake wanne walikuwa mbali kabisa; ng’ambo ya pili ya Pasifiki, wakicheza ‘mariachi’ (muziki wa asili) na ‘campesinos’ (wakulima) katika milima ya Sierra Madre Occidental huko Sinaloa – na kulala na wanawake warembo, wenye bikini, wanaokunywa martini, Acapulco nchini Meksiko.

Watu wanaohatarisha maisha yao kwa kudharau sheria wakati mwingine hawatakiwi kudharauliwa. Ni sawa na mtu aliyepoteza kila kitu katika maisha yake. Wana uwezo wa kufanya chochote. Serikali ya Meksiko ilipokataa kukidhi matakwa ya El Tigre ya kubadili katiba ya nchi – kuondoa kipengele cha mkataba wa kubadilishana watuhumiwa na washtakiwa – ili akikamatwa asipelekwe Marekani ambako atafungwa na kufia gerezani, El Tigre aliilaani Serikali ya Meksiko.

Kujibu mapigo, ya laana ya maluuni, Serikali ya Meksiko ikawakabidhi makamanda 7 wa Kolonia Santita kwa mamlaka za Marekani, na kuongeza juhudi za kumsaka El Tigre mpaka nje ya Amerika ya Kusini na Kaskazini.

El Tigre, kuikomoa serikali na kuwalipia kisasi makamanda wote waliouwawa na kufungwa na shirikisho, akamuua Mwanasheria Mkuu wa Serikali (PGR) na maafisa 7 wa Jeshi la Polisi la Nchi (PJF) kulinganisha idadi ya makamanda wake waliopelekwa Marekani – halafu ‘akapotea’, kabisa; baada ya kutangaza vita na Serikali ya Meksiko.

Tume ya Dunia imekuwa ikimtafuta Chui wa Siberia kwa zaidi ya miaka tisa. Bila mafanikio. Ulinzi wa Panthera Tigrisi ni wa kimataifa. Mbali na kulindwa na wananchi wa Oaxaca (kwa sababu ya kuwajengea shule, hospitali, makanisa, misikiti na kadhalika), na polisi wa shirikisho (kwa sababu ya vitisho, mauaji na rushwa); El Tigre analindwa na jeshi binafsi la kujihami (‘autodefensa’) la wanajeshi wastaafu zaidi ya 1300.

Mbali hali kadhalika na autodefensa; kiongozi wa Kolonia Santita ana walinzi binafsi makomandoo (48) akiwemo A. Narochnitskaya Belinsky, mtaalamu wa kutengeneza nyambizi wa Urusi, na Nicolas Kahima Kankiriho (‘Kahima the Warrior’) mwanajeshi wa kulipwa wa Uganda – aliyetoroka na El Tigre katika nyambizi ya Jefe de Jefes SPD (‘the Silent Predator of the Deep’), iliyotengenezwa na Belinsky, katika Ghuba ya Meksiko Septemba 16, 1986.

Kolonia Santita (KS-14) ni genge hatari kuliko yote la madawa ya kulevya katika eneo lote la Hemisifia ya Magharibi. Lilianzishwa mwaka 1980 kwa kuunganisha magenge saba ya madawa ya kulevya ya Amerika, Meksiko na Kolombia, na magenge mengine madogomadogo zaidi ya tisini ya Amerika ya Kusini na Kaskazini.

Genge hili kubwa, pengine kuliko yote duniani, lilianzishwa na watu kumi na nne kwa lengo la kujiimarisha kibiashara ndani na nje ya Hemisifia ya Magharibi (na kupanua wigo wa biashara yao kimataifa – kuanzia Hemisifia ya Magharibi mpaka ya Mashariki, Kusini na Kaskazini).

Magenge hayo ni Baja California, Matamolos, Guanajuato (Meksiko), The Benson Brothers of Chicago, The Family (Marekani) na Cartagena na Diablos de Amazonas au Mashetani wa Amazoni (Kolombia).

Benson Bennett Stansfield (‘El Tigre’) wa Marekani, Gortari Manuel (‘El Padrino’) wa Meksiko na Eduardo Chapa de Christopher (‘El Chupacabra’) wa Kolombia ndiyo wakurugenzi waanzilishi wa KS-14.

Wengine ni Ignacio Leonardo de la Fuente, Marciano Moreno Herrera – Hana uhusiano na mchumba wa Debbie, Giovanni Gonzalez Murillo, Herrera Monteagudo, Panceano Nieto, Raymundo Escoto Martinez (kutoka Meksiko), José Alberto Araújo, Victor Miguel Enrique, Javier Ricardo Antonio, Carlos Pulecio Alcántara, Roberto Mosquera Portocarrero (kutoka Kolombia) na Freeman Boyd Figueroa kutoka Amerika.

No comments:

Post a Comment

Roho Yako

289. Roho yako inatoka wapi? Ya kwangu inatoka Tanzania. Kwa sababu amani na utulivu ndivyo vitu vya muhimu zaidi katika maisha yangu. ...