Msomaji
 wa kawaida wa hadithi au maandiko yoyote hajali iwapo anachokisoma 
kimeandikwa kwa utaalamu au la – hakuna atakayejali iwapo kanuni za 
fasihi zitavunjwa ili kupendezesha hadithi au maandiko yoyote. Wengi 
wanachojali ni utamu wa hadithi wanayoisoma, si kanuni za fasihi 
zilizotumika katika maandalizi ya hadithi hiyo. Lakini hayo yanaweza 
kusamehewa. Kisichoweza kusamehewa ni tahajia, sarufi au matumizi ya 
mazungumzo ya kawaida ya mtaani katika maandiko ya hadithi. 
Hupaswi
 kuandika mambo ya kihuni au utani katika hadithi itakayosomwa na watu 
wengi kwani wengine hawapendi utani au uhuni hasa wale waliotoa pesa zao
 kununua hadithi wakitarajia kupata la maana isipokuwa katika hadithi za
 vichekesho peke yake. Hadithi za vichekesho peke yake ndiyo unaweza 
kuandika chochote unachojisikia kuandika. Andika mambo ya kihuni au 
utani ndani ya funga na fungua semi ionekane si wewe uliyesema bali 
wahusika wako katika hadithi. 
Usiangalie
 tu nani atasoma hadithi yako leo, bali angalia nani atasoma hadithi 
yako miaka mia moja ijayo. Na kumbuka, huwezi kumdanganya msomaji. 
Usiandike kosa kwa makusudi ukidhani msomaji hatagundua. Anaweza 
kugundua, na akigundua anaweza asiwe shabiki yako tena katika hadithi 
zako zitakazofuata. 
Kanuni
 maarufu katika fasihi ni “Onesha, usiambie”. Ukisema “John alikuwa na 
furaha,” unamtaarifu msomaji kwamba John alikuwa na furaha. Lakini 
ukisema “John alitabasamu,” unampa msomaji akili itakayofanya ajue kama 
John alikuwa na furaha. Unamwonesha, humwambii! Kanuni hii ni nzuri 
katika fasihi na ndivyo mambo yalivyo katika maisha ya kila siku. Kama 
John ni mfanyakazi mwenzako, hatuna mtu wa kutuambia kama John ana 
furaha kwa sababu ya kupandishwa cheo au mshahara. Tunachotakiwa kufanya
 ni kuchunguza vizuri tabia ya John na kujua nini kinaendelea katika 
maisha yake. Kuonesha humfanya msomaji azame katika hadithi – hufanya 
hadithi ionekane ya kweli – hasa mwandishi anapounganisha vyema ubunifu 
na uhalisia. 
Kanuni
 za fasihi ndiyo msingi wa maandiko yote ya kitaalamu hapa ulimwenguni. 
Watu hawana budi kuzifuata kanuni hizo iwapo wanataka kutumia vipaji 
vyao katika ngazi ya kimataifa. 

Mambo ya kihuni au utani ni kama vile misimu au simo (‘slang’) au lugha za mitaani, au matusi.
ReplyDelete