Sunday, 4 December 2016

Kanuni za Fasihi Ndiyo Msingi wa Maandiko Yote ya Kitaalamu Hapa Ulimwenguni

Msomaji wa kawaida wa hadithi au maandiko yoyote hajali iwapo anachokisoma kimeandikwa kwa utaalamu au la – hakuna atakayejali iwapo kanuni za fasihi zitavunjwa ili kupendezesha hadithi au maandiko yoyote. Wengi wanachojali ni utamu wa hadithi wanayoisoma, si kanuni za fasihi zilizotumika katika maandalizi ya hadithi hiyo. Lakini hayo yanaweza kusamehewa. Kisichoweza kusamehewa ni tahajia, sarufi au matumizi ya mazungumzo ya kawaida ya mtaani katika maandiko ya hadithi.

Hupaswi kuandika mambo ya kihuni au utani katika hadithi itakayosomwa na watu wengi kwani wengine hawapendi utani au uhuni hasa wale waliotoa pesa zao kununua hadithi wakitarajia kupata la maana isipokuwa katika hadithi za vichekesho peke yake. Hadithi za vichekesho peke yake ndiyo unaweza kuandika chochote unachojisikia kuandika. Andika mambo ya kihuni au utani ndani ya funga na fungua semi ionekane si wewe uliyesema bali wahusika wako katika hadithi.

Usiangalie tu nani atasoma hadithi yako leo, bali angalia nani atasoma hadithi yako miaka mia moja ijayo. Na kumbuka, huwezi kumdanganya msomaji. Usiandike kosa kwa makusudi ukidhani msomaji hatagundua. Anaweza kugundua, na akigundua anaweza asiwe shabiki yako tena katika hadithi zako zitakazofuata.

Kanuni maarufu katika fasihi ni “Onesha, usiambie”. Ukisema “John alikuwa na furaha,” unamtaarifu msomaji kwamba John alikuwa na furaha. Lakini ukisema “John alitabasamu,” unampa msomaji akili itakayofanya ajue kama John alikuwa na furaha. Unamwonesha, humwambii! Kanuni hii ni nzuri katika fasihi na ndivyo mambo yalivyo katika maisha ya kila siku. Kama John ni mfanyakazi mwenzako, hatuna mtu wa kutuambia kama John ana furaha kwa sababu ya kupandishwa cheo au mshahara. Tunachotakiwa kufanya ni kuchunguza vizuri tabia ya John na kujua nini kinaendelea katika maisha yake. Kuonesha humfanya msomaji azame katika hadithi – hufanya hadithi ionekane ya kweli – hasa mwandishi anapounganisha vyema ubunifu na uhalisia.

Kanuni za fasihi ndiyo msingi wa maandiko yote ya kitaalamu hapa ulimwenguni. Watu hawana budi kuzifuata kanuni hizo iwapo wanataka kutumia vipaji vyao katika ngazi ya kimataifa.

1 comment:

  1. Mambo ya kihuni au utani ni kama vile misimu au simo (‘slang’) au lugha za mitaani, au matusi.

    ReplyDelete

Roho Yako

289. Roho yako inatoka wapi? Ya kwangu inatoka Tanzania. Kwa sababu amani na utulivu ndivyo vitu vya muhimu zaidi katika maisha yangu. ...