195. Sipendi dharau: mimi kumdharau mtu au mtu kunidharau mimi. 
Sitakudharau kwa sababu sikujui. Hupaswi kunidharau kwa sababu hunijui.
Mzazi
 hamjui mtoto wake na mtoto hamjui mzazi wake. Kila mtu hapa duniani ni 
wa kipekee na wanasayansi wanatuambia kuwa tuko peke yetu hapa 
ulimwenguni. Lazima tujifunze kupendana na kuheshimiana. 
 
 Mama mmoja alimpenda sana mtoto wake hata akatoa jicho lake moja
 na kumpa mwanaye ambaye alipata ajali ya gari akiwa mdogo na kupofuka 
jicho moja. Mama na mtoto na mume wake walikuwa wakitokea Dumila, 
Morogoro, lakini walipofika Gairo gari lao dogo lilipinduka, lakini 
baadaye mume akafariki alipokuwa hospitalini Dodoma. Mama alikuwa na 
mapenzi yasiyokuwa na masharti yoyote kwa mtoto wake, na mtoto 
alionyesha mapenzi yasiyokuwa na masharti yoyote kwa mama yake. 
 
 Baada ya kumaliza masomo, kidato cha sita katika Shule ya Sekondari ya 
Mazengo iliyokuwa pembezoni kidogo mwa mji wa Dodoma, mtoto alikwenda 
Ulaya kwa masomo zaidi. Akiwa huko akaoa lakini akamsahau kabisa mama 
yake pamoja na ndugu zake wote. Si kwa simu, si kwa barua, si kwa pesa! 
Miaka mingi baadaye mama akawa amemkumbuka sana mtoto wake hata akaamua 
kujichanga na akafanikiwa kupata hati ya kusafiria na viza kwenda Ulaya 
kumtafuta mwanaye. Ulaya kuna Watanzania ambao huyo mama aliwafahamu, 
kupitia kwa waumini wenzake wa kanisa la Wasabato la Dodoma. Watanzania 
hao walimsaidia kusafiri kwa maana ya udhamini na tiketi ya ndege, kwani
 hata wao hawakupendezwa na tabia ya Mtanzania mwenzao. Alipofika 
Lasembagi, ambapo ndipo mwanaye alikuwa akiishi na mke wa Kifaransa na 
watoto wao wawili, mama alielekezwa nyumbani kwa mwanaye na akachukuliwa
 teksi ambayo ilimpeleka moja kwa moja mpaka kwenye anuani ya nyumba 
yake. Cha kushangaza, yule mtoto akamkana mama yake na akamfukuza kama 
mbwa na mama akaondoka huku machozi yakimtoka katika jicho lake moja. 
 
 Miaka mitatu baadaye yule mtoto alikuja Tanzania kutalii akiwa na mke 
na watoto wao wawili. Wakiwa Dar es Salaam, watu wakampa taarifa za 
msiba wa mama yake. Nafsi ilimsuta. Hata mke wake nafsi ilimsuta pia! 
Walipotoka Manyara, ambapo walikwenda kuangalia wanyama, mke akamsihi 
mume wakahani msiba wa mama yake. Hivyo, wakasafiri kwenda Dodoma. 
Walipofika Area C, nyumbani kwa mama yake, walikutana na majirani. Mama 
mmoja akamkabidhi yule mtoto barua aliyopewa na marehemu ili amkabidhi 
palipo majaaliwa. 
 
 Barua ilikuwa na ujumbe mzito na wa 
kusikitisha. Mama alimwomba radhi mtoto wake kwa makosa yoyote ambayo 
labda aliwahi kumfanyia. Hakukumbuka kama aliwahi kumfanyia mwanaye 
makosa ya aina yoyote ile licha ya kumchapa, kwa faida ya mtoto mwenyewe
 ya baadaye. Barua ilikuwa ndefu. Lakini ilimalizia kwa kusema, 
“Nilikupenda mwanangu, nakupenda hata sasa, na nitakupenda daima. Siku 
yoyote Mungu atakapokupa neema ya kurudi, kama nitakuwa hai, 
nitakuchinjia kuku; kama nitakuwa nimekufa, nitatumia mifupa yangu 
kukukumbatia.” 
 
 Yule mama hakuwa na makosa. Mtoto alikuwa na 
makosa. Lakini hawa walikuwa ni watu wawili tofauti, kabisa! Mama 
hakumjua mtoto wake, na mtoto hakumjua mama yake. Mama hakujua kama 
mtoto wake alikuwa na akili ya kumgeuka. Mtoto hakujua kama mama yake 
alimpenda kwa dhati! 
 
 Kuna nguzo saba ambazo hazina budi 
kuzingatiwa kama unataka kuheshimiwa na kuwaheshimu wengine. Kwanza 
kabisa jitambue: wewe ni nani na unafanya nini hapa duniani. Halafu, 
kabla ya kusema jambo lolote kwa mtu yoyote fikiria kwanza maana au 
madhara ya hilo unalotaka kulisema. Kisha jifunze tamaduni mbalimbali na
 watendee wengine kama vile unavyotaka kutendewa au kama vile 
wanavyotaka kutendewa. Jifunze kusamehe na kusuluhisha migogoro katika 
jamii unamoishi huku ukidumisha heshima na utu kwa binadamu wenzako. 
Jijengee imani kwa watu, punguza upendeleo, fanya kazi kama timu kwani 
hakuna ‘mimi’ katika umoja ila kuna ‘sisi’, na jitahidi kwa kadiri ya 
uwezo wako WOTE kwa manufaa ya wote. Kuwa kiongozi katika kila jambo 
unalofanya na katika kila kitu unachofanya. Jitahidi kufanya jambo au 
kitu kwa usahihi kwa kadiri utakavyoweza. 
 
 Migogoro inatokea 
kwa sababu watu wameshindwa kuheshimiana. Ukijiheshimu na ukaheshimu 
wengine, utaacha dunia katika hali nzuri kuliko ulivyoikuta. 
http://www.facebook.com/koloniasantita
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
Roho Yako
289. Roho yako inatoka wapi? Ya kwangu inatoka Tanzania. Kwa sababu amani na utulivu ndivyo vitu vya muhimu zaidi katika maisha yangu. ...
- 
KITENDAWILI CHA KOLONIA SANTITA Shilingi milioni moja za Kitanzania kushindaniwa ndani ya miezi sita kuanzia leo Swali: Kila namba ...
 - 
Mpelelezi wa Tume ya Dunia kutoka Jerusalem, Israeli, Kanali Daniel ‘Yehuda Ben-Asher’ Ebenezer, Daniel Yehuda, alikuwa komandoo wa kit...
 


Ukitaka kuwa na mahusiano mema na watu wa muhimu katika maisha yako, waheshimu. Heshima yako itakulipa!
ReplyDeleteTuko peke yetu ulimwengu mzima halafu bado tunagombana na kudharauliana!
ReplyDelete