Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Benito Juárez wa Mexico City ni uwanja wa ndege mkubwa kuliko vyote Mexico City, na uwanja wa ndege wa nyumbani wa Kolonia Santita. Maelfu ya vidae (‘mules’) wa Kolonia Santita hupitia hapo kila mwezi kusafirisha madawa na fedha – kwenda na kurudi nje na ndani ya Mexico City.
Kolonia Santita, kwa kutumia wasafirishaji wadogowadogo wa madawa ya kulevya wanaojulikana kwa lugha ya kigeni isiyo rasmi kama ‘mules’ (vidae – Kamusi ya Enock Maregesi), husafirisha maelfu ya kilo za madawa ya kulevya kila mwezi; kila kidae akiwa na kilo moja au zaidi tumboni mwake (au ndani ya sanduku lake).
Saa arobaini na nane kabla ya Vijana wa Tume ‘kutua’ Mexico City, viwanja vyote vya ndege vya Mexico City – vikiwemo vyote viwili vya Benito Juárez – vilidhibitiwa vikali na majeshi haramu ya Kolonia Santita ya ‘autodefensa’ na ‘sicarios’, hadi waliposhtuliwa na simu ya katibu muhtasi wa Panthera Tigrisi Maria Cosillas Ortega. Mtu mmoja ‘aliyefanana’ na John Murphy alikuwa ofisini kwa El Tigre akitafuta nyaraka za siri, katika mazingira ambayo Maria hakuyaelewa.
Sehemu nyingi za Mexico City zikiwa zimedhibitiwa vikali kwa bunduki hatari za Kirusi za AK-74 na AK-47, na za Kibelgiji za FNP90 zenye uwezo wa kutoboa kinga ya risasi, wanajeshi wa Kolonia Santita walikuwa wakijidanganya (sana) kuwasubiri Vijana wa Tume katika viwanja vya ndege. Kwa mbinu za WODEC-Intelligence na FAM, Vijana wa Tume waliingia Mexico City usiku wa manane – kama wagonjwa mahututi kutoka Guadalajara.
No comments:
Post a Comment