Thursday 22 June 2017

Simama Juu ya Mabega ya Mapandikizi ya Watu

Msamaha si kwa ajili ya watu wenye mabawa ya kuku, ni kwa ajili ya watu wenye macho ya tai.

Macho ya tai yana nguvu mara nne zaidi ya macho ya mwanadamu. Tai ana uwezo wa kuona hadi umbali wa kilometa themanini bila matatizo yoyote. Ana uwezo wa kuruka hadi futi elfu kumi, na ana uwezo wa kukimbia hadi mwendokasi wa kilometa mia moja na ishirini kwa saa.

Kihekima, wale tu wanaoweza kuona mbali kama tai ndiyo watakaouweza msamaha. Lakini wale wenye mabawa ya kuku, wale ambao hawawezi kuruka wala kuona mbali, watapata taabu sana kuijua radhi. Kwa hiyo, wanapaswa kukua. Ukiwa mnyenyekevu wa moyo hutamchukia adui yako.

Msamaha si jambo dogo. Watu wadogo, watu wenye uwezo mdogo wa kufikiri, hawawezi kupambana na changamoto za msamaha. Msamaha ni kwa ajili ya watu wenye macho kama ya tai wanaoweza kuona mbali ambao wako tayari kushindwa vita ili washinde vita.

Hewa inaingia ndani ya mapafu na kutoka; chakula kinaingia ndani ya mwili na kutoka; mwanamasumbwi anapigana bila kugombana; injini ya gari haiwezi kusukuma gari mbele au nyuma bila kutoa hewa katika paipu ya ekzosi. Lakini kile kinachoingia moyoni mwako hakitoki! Maumivu yanapoingia ndani ya moyo yanapaswa kutoka nje kama yalivyoingia kwa sababu, yasipotoka yatatengeneza sumu ndani ya moyo wako na yatatengeneza sumu ndani ya roho yako pia.

Sumu hiyo itahatarisha safari yako ya mbinguni na Mungu hatakusamehe tena. Badala ya yule aliyekukosea kuumia, utaumia wewe uliyekosewa. Yesu anaposema samehe saba mara sabini hatanii. Usiposamehe, hutasamehewa.

No comments:

Post a Comment

Roho Yako

289. Roho yako inatoka wapi? Ya kwangu inatoka Tanzania. Kwa sababu amani na utulivu ndivyo vitu vya muhimu zaidi katika maisha yangu. ...