Eksitasi na methi ni biashara kuu ya tatu ya Kolonia Santita baada ya
kokeini na heroini. Maabara ya kutengenezea eksitasi na methi ya
Kolonia Santita (inayoitwa ‘maquiladora’ au kiwanda cha uzalishaji)
yenye uwezo wa kutengeneza vidonge 17,000 vya eksitasi kwa saa na tani
20 za methi kwa mwezi, zenye thamani ya mtaani ya shilingi trilioni moja
za Kitanzania, ni kubwa kuliko zote katika Jimbo la Sinaloa.
Ndani
ya methi kuna LSD (ambayo ni ‘Lysergic acid diethylamide’ – au
‘Laisajiki asidi dayatholamaidi’ kwa Kiswahili chepesi). Ndani ya
eksitasi kuna MDMA (‘Methylenedioxymethamphetamine’ – au
‘Metholini-dayoksi-meth-amfetamini’ kwa Kiswahili chepesi). Hizi ni
kemikali za taswira za kiwendawazimu.
Eksitasi, MDMA, au Furaha –
Kamusi ya Enock Maregesi – ni vidonge vinavyotokana na madawa
yanayotengeneza methamfetamini, vilivyotengenezwa kwa mara ya kwanza na
Mkemia Fritz Harber mnamo mwaka 1898 huko Ujerumani (lakini vikapewa
kibali rasmi na serikali mnamo mwaka 1914) na ambavyo leo hii vimekuwa
na umaarufu mkubwa hususan katika majumba ya starehe ya Ulaya na
Amerika. Koka hutengeneza kokeini. Afyuni hutengeneza heroini.
‘Ephederine’ au ‘afedrini’ hutengeneza methi. Sassafrasi hutengeneza
eksitasi.
Mafuta ya sassafrasi (‘sassafrass’) yamekuwa malighafi
muhimu sana katika utengenezaji wa viungo vya chakula, manukato ya
wanawake na wanaume na dawa za kuulia wadudu kwa karne nyingi. Kiungo
kikuu cha mafuta ya sassafrasi ni safro (‘safrole’) ambayo kikemia
huweza kugeuzwa na kuwa ‘isosafrole’. Safro na ‘isosafrole’ hutumika
kama malighafi ya mwanzo kabisa katika utengenezaji wa eksitasi.
Safro
ilitumiwa kwa mara ya kwanza kama malighafi ya eksitasi na mkemia wa
Kijerumani Fritz Habar mnamo mwaka 1898; lakini kidonge halisi cha
eksitasi kilikuwa hakijatolewa kibali mpaka mwaka 1914, kampuni ya
madawa ya Merck iliporuhusiwa kisheria kukitengeneza.
Eksitasi
inaweza kutengenezwa kirahisi mno kwa kutumia safro, na bei yake ni
ndogo sana kulinganisha na baadhi ya madawa kama kokeini na heroini.
Kwa
mujibu wa ripoti ya mwaka ya Kituo cha Uangalizi wa Madawa na Uraibu wa
Madawa cha Bara la Ulaya (EMCDDA – ‘European Monitoring Centre for
Drugs and Drugs Addiction’), uzalishaji wa eksitasi na methi waweza
kukadiriwa kufikia mpaka tani 520 kwa mwaka duniani kote.
Eksitasi
huzalishwa zaidi barani Ulaya, huku Uholanzi ikiwa ya kwanza kwa
uzalishaji, na pia Kusini Mashariki mwa Asia (China, Indonesia, na Hong
Kong) na Amerika ya Kaskazini.
Kwa mujibu wa ripoti hiyohiyo ya
EMCDDA, tani 8.5 za eksitasi zilikamatwa mwaka 2004 katika operesheni ya
dunia nzima; asilimia 50 ya hizo ikitoka Ulaya ya Kati (na Magharibi),
23 ikitoka Amerika ya Kaskazini, na 16 ikitokea Oshania (‘Oceania’).
Bei
ya wastani ya kidonge cha eksitasi mwaka 2004 ilikuwa karibu shilingi
6,000 za Kitanzania nchini Polandi na nchi za Mashariki, na shilingi
30,000 – 50,000 za Kitanzania nchini Ugiriki na Italia.
Malighafi,
kama vile mafuta ya sassafrasi, inayotumika kutengeneza eksitasi na
aina zingine za methi, hufikirika mara nyingi kutumiwa na mamafia wa
madawa ya kulevya. Kukomesha na kuzuia biashara isiyo halali ya
eksitasi, mamlaka za kimataifa zimeunda sheria na taratibu za
kiushirikiano za udhibiti wa kemikali tangulizi (‘precursors’) za
eksitasi; na kemikali zingine zinazotumika katika uchakataji wa
uzalishaji wa sassafrasi.
Mafuta ya sassafrasi hupatikana kutoka
katika mizizi na matawi ya aina mbalimbali ya miti. ‘Sinamomamu
Pathenoksiloni’ (‘Cinnamomum Parthenoxylon’) kwa mfano, ni mmea kutoka
Indochina wenye kiwango kikubwa cha safro – ambao sasa umejumuishwa
katika kitabu chekundu cha Umoja wa Kimataifa wa Hifadhi ya Maliasili
(au IUCN kwa kifupi).
Huu si mfano pekee unaoweza kutajwa na
wadau. China ni mteja mkubwa wa mafuta ya sassafrasi, kuliko nchi zote
duniani, ikiwa imefikisha mpaka kiwango cha matumizi ya tani 2000 kwa
mwaka – kwa ajili ya kutengeneza kemikali ya manukato na viungo iitwayo
‘heliotropine’ na bidhaa zingine.
Vyanzo vya mafuta ya sassafrasi
vimekuwa vigumu sana kupatikana siku hizi kutokana na sheria kali za
mamlaka, na jitihada za serikali katika kuzuia ukataji miti ovyo katika
misitu ya ukanda wa joto. China, Brazili na Vietnamu – ambao ndiyo
wazalishaji wakuu wa mafuta ya sassafrasi – zimepiga marufuku ukataji
miti ili kuzuia uhaba wa miti kwa jumla.
Brazili ndiyo ilikuwa
nchi ya kwanza kuzuia mavuno ya miti ya sassafrasi mwaka 1990. Kisha
Vietnamu ikachukua nafasi ya Brazili kama mzalishaji; lakini mnamo mwaka
1999, Vietnamu nayo ikazuia mavuno; huku usafirishaji wa sassafrasi nje
ya nchi ukisimama kabisa mnamo mwaka 2000. Mpaka kufikia mwaka 2003,
Vietnamu ilikuwa ikifuata sera ya kuingiza sassafrasi nchini mwake na
kuisafirisha tena kwenda nchi za nje.
Kuanzia mwaka 2003
uzalishaji ulihamia nchini Kambodia katika Milima ya Cardamom
inayodhibitiwa na Khmer Rouge (chama cha kikomunisti cha Kampuchea,
Kambodia), lakini miaka michache tu baadaye (kuanzia mwaka 2005)
serikali ya Kambodia ikapiga marufuku uvunaji wa miti inayotoa
sassafrasi hali kadhalika – ambayo sasa inajulikana zaidi kama miti
iliyoko hatarini sana kupotea.
Kimsingi sheria ya usimamishaji wa
uzalishaji haikufanya kazi sawasawa. Tangu mwaka 2005 zaidi ya tani 600
za mafuta zilizalishwa na kusafirishwa nje ya nchi. Sheria kali zaidi
kutoka serikalini – ikisaidiwa na Mamlaka ya Kudhibiti Madawa ya Kulevya
Nchini Marekani DEA – ilipelekea kukamatwa kwa makontena matatu (kwenye
bandari ya Tailandi Oktoba 2007) yaliyokuwa na tani 50.4 za safro,
zilizokuwa tayari kusafirishwa kwenda Amerika na China.
Mwaka 2008
(Juni) ushirikiano wa mamlaka za Kambodia na jeshi la polisi la
Australia ulizuia na kukamata tani 33 za mafuta ya safro, zilizokuwa na
uwezo wa kutengeneza vidonge milioni 245 vya eksitasi. Kwa mujibu wa
azimio la Ubalozi wa Australia nchini Kambodia, vidonge hivyo vilikuwa
na thamani ya mtaani ya shilingi trilioni 11.8 za Kitanzania. Mafuta
hayo yaliharibiwa na serikali ya Kambodia kwa kuyachoma moto katika
kipindi cha siku tatu mfululizo, chini ya usimamizi wa jeshi la polisi
la Australia.
Mamlaka za Kambodia zimekuwa zikifanya kazi usiku na
mchana toka mwaka 2002 kuzuia uzalishaji wa mafuta ya safro; na tangu
kipindi hicho zimefanikiwa kugundua na kuharibu zaidi ya maabara 50 za
siri, zilizokuwa na uwezo wa kuzalisha hadi galoni 15 za mafuta kwa siku
kwa mujibu wa jeshi la polisi la Australia.
Uzalishaji wa mafuta
ya sassafrasi nchini China unadhibitiwa vikali na serikali, lakini
makampuni ya Kichina (na hata yale ya Kivietnamu) hufanya shughuli zake
nchini Laosi na Bama katika vipindi tofautitofauti. Biashara ambayo
makampuni hayo yanafanya si halali; lakini pamoja na hilo, tani chache
za mafuta ya safro kutoka katika maeneo hayo huingia nchini China mara
kwa mara kwa njia za kimafia.
Ndani kabisa ya Milima ya Cardamon
na Hifadhi ya Taifa ya Phnom Samkos huko magharibi mwa Kambodia, viwanda
vya siri vinatengeneza mafuta ya safro kwa ajili ya kutengeneza vidonge
vya eksitasi. Matokeo yake serikali ya Kambodia inalipa gharama kubwa
kwa maana ya mazingira.
Miti yenye mafuta ya safro, yanayofanana
na mafuta ya samli kwa kiasi fulani, hukatwa wakati wa uchakataji wa
uzalishaji (‘manufacturing process’). Mizizi ya miti hiyo, pamoja na
matawi, ambayo ndiyo sehemu hasa yenye mafuta ya safro, hukatwa kwa
misumeno ya umeme na baadaye kuchemshwa ndani ya mapipa makubwa ya
chuma. Kimiminika kinachotokea baada ya hapo huchujwa kitaalamu
(‘distilled’) juu ya mioto inayohitaji kiasi kikubwa mno cha kuni kuweza
kuichochea.
Uzalishaji wa mafuta ya safro ni biashara kubwa.
Hivyo ukataji mkubwa wa miti, na mmomonyoko wa ardhi, uharibu kabisa
sehemu za milimani zinazozunguka viwanda.
Mabaki ya mapipa na
vifaa vyote vinavyotumika katika utengenezaji wa safro ni hatari kwa
afya ya binadamu; na milipuko hutokea mara kwa mara. Mifereji ya jirani
inayoleta maji kwa ajili ya upishi wa mafuta ya sassafrasi, muda si
mrefu nayo huziba – kutokana na uchafu wa viwandani na hivyo kuathiri
kabisa mazingira ya kibiolojia (‘ecosystem’) ya maeneo hayo. Hata mafuta
yenyewe si salama. Mafuta ya sassafrasi huweza kusababisha ugonjwa wa
saratani, na eksitasi husababisha sumu katika mishipa ya damu ya
serotonini.
Pamoja na kwamba uzalishaji mdogo mdogo wa mafuta ya
safro umekuwa ukiendelea kwa muda mrefu nchini Kambodia kwa ajili ya
madawa ya kienyeji, na kwa ajili ya shughuli za kisayansi na tafiti za
kitabibu, uzalishaji mkubwa wa mafuta ya safro kwa ajili ya biashara ya
madawa ya kulevya umekuwa ukipungua – tangu mwishoni mwa miaka ya
tisini.
Katika miaka ya hivi karibuni, mamlaka zimechukua hatua
kali dhidi ya biashara ya safro; ikiwa ni pamoja na uvamizi wa hali ya
juu wa kipolisi – kuwakumbusha watu kwamba, biashara ya safro
itawapeleka jela. Uvamizi wa tarehe 12/6/2009 uliofanywa na taasisi
isiyokuwa ya kiserikali inayojihusisha na hifadhi ya mazingira ya Flora
and Fauna International, kwa kushirikiana na mamlaka za Kikambodia,
walikamata madumu 142 yaliyokuwa na tani 5.7 za mafuta ya sassafrasi.
Shehena hiyo, iliyokamatwa nyumbani kwa mtu katika kijiji cha O' Kambou,
magharibi mwa milima ya Cardamom, ilikuwa na uwezo wa kuzalisha vidonge
milioni 44 vya eksitasi; vyenye thamani ya mtaani ya shilingi trilioni
1.94 za Kitanzania.
Viwanda vingi vya mafuta ya safro vinaweza
kupatikana katika Hifadhi ya Taifa ya Wanyamapori ya Phnom (‘Fnam’)
Samkos, ambayo inapatikana katikati ya Milima ya Cardamom na ambapo
ndipo miti mingi ya sassafrasi inapopatikana.
Milima ya magharibi
ya Cardamom ni sehemu ya ukanda mkubwa kuliko yote wa msitu wa mvua
katika eneo la Kusini Mashariki mwa Asia; na ni makazi ya aina zaidi ya
themanini za wanyama zilizoko mbioni kupotea; kama vile chui, tembo na
mamba.
Mafuta ya safro, ambayo pia hutumika katika utengenezaji wa
vipodozi na madawa ya kienyeji ya waasi wekundu (‘rouge’) wa Khmer,
yanazalishwa kutoka katika mafuta ya mti unaojulikana kwa Kikhmer kama
‘Mreath Prew Phnom’ – ambao wataalamu hudhani ni Sinamomamu
Pathenoksiloni (au ‘Cinnamomum Parthenoxylon’).
Aina hiyo ya miti
inasemekana kuwa chache mno duniani, na nchini Vietnamu, imewekwa katika
kundi la miti iliyoko hatarini sana kupotea. Mti wa Sinamomamu
Pathenoksiloni hauna jina kamili kwa Kiingereza au Kiswahili, na hakuna
mtu ajuaye ni miti kiasi gani ya namna hiyo imebaki duniani.
Miti
minne ya ‘Mreath Prew Phnom’ hutakiwa kuzalisha pipa moja la galoni
arobaini la mafuta ya safro, na miti mingine sita ambayo haina umuhimu
sana hukatwa na kutumika kama kuni – kwa ajili ya mti mmoja wa ‘Mreath
Prew Phnom’!
Wafanyakazi wanaopika na kuchuja mafuta ndani kabisa
ya misitu, kadhalika hutegemea mawindo ya wanyama adimu wa msituni (kama
kakakuona, tausi, chatu, duma na chui) kwa ajili ya chakula au kipato
katika masoko kadha wa kadha ya wanyamapori. Uwindaji wa wanyama
uhatarisha maisha ya wawindaji zaidi ya 15,000 wanaokaa pembezoni mwa
hifadhi hizo za wanyama.
Kwa bahati mbaya mahitaji ya eksitasi na
mafuta ya sassafrasi na mafuta ya safro, kwa ajili ya matumizi ya
viwandani, bado hayajapungua hata kidogo. Kukidhi haja ya mahitaji ya
leo ya mafuta haya, misitu ya ukanda wa joto wa dunia hii hupoteza miti
kadiri ya 500,000 kwa mwaka. Miti hii haitoki mashambani, la hasha!
Inatoka katika misitu ya asili ya China, Brazili, Vietnamu, na sasa
Kambodia; licha ya juhudi za hizi nchi za kupiga marufuku uvunaji wa
miti yenye mafuta ya sassafrasi au safro, na uchujaji wake kwa ajili ya
kuzalisha mafuta.
Kutoka katika misitu mikubwa ya Kambodia,
Vietnamu, Brazili na China, mpaka katika majumba ya starehe ya duniani
kote; eksitasi itaendelea kuburudisha watu duniani – na mamafia
wataendelea kufanya biashara haramu – iwapo watu hawatasimama kidete,
kusema vidonge vya burudani sasa basi.
Eksitasi ni ngumu sana
kudhibitiwa na serikali peke yake. Udogo wake (udogo wa umbo lake)
hufanya iwe rahisi sana kulanguliwa na mamafia; na viwanda huweza
kuhamishika kirahisi (kutoka msitu mpaka msitu au nchi mpaka nchi)
kukwepa vyombo vya dola na taasisi za kimataifa.
Wataalamu wengi
(hususan Wafaransa) wametahadharisha umma juu ya eksitasi, na madhara ya
muda mrefu ya madawa hayo katika ubongo. Magonjwa mengi yanayohusiana
na eksitasi ni mabaya. Unaweza kuugua kansa, mawazo na ugonjwa wa akili.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
Roho Yako
289. Roho yako inatoka wapi? Ya kwangu inatoka Tanzania. Kwa sababu amani na utulivu ndivyo vitu vya muhimu zaidi katika maisha yangu. ...
-
Mercury Cougar ya John Murphy aliyonunua mwaka 1990 kwa gharama kubwa huko Michigan nchini Marekani. Gari hilo lililorekebishwa kwa ajili ...
-
Siku ya kuzaliwa ni siku ya kwanza ya safari nyingine ya siku 365, saa 5, dakika 48, sekunde 46 na maili milioni 600 kulizunguka jua. Safi...
-
KITENDAWILI CHA KOLONIA SANTITA Shilingi milioni moja za Kitanzania kushindaniwa ndani ya miezi sita kuanzia leo Swali: Kila namba ...
No comments:
Post a Comment