Monday, 12 December 2016

Upendo wa ‘Agape’

203. Kuna aina tatu za upendo hapa ulimwenguni. Kuna upendo wa ‘agape’, upendo kati ya Mungu na binadamu na kati ya binadamu na binadamu mwenzake lakini hao binadamu shuruti wawe marafiki wa msalaba wa Yesu Kristo. Aidha kuna upendo wa ‘phileo’, upendo kati ya mtu na mtu au kati ya mtu na kitu au kati ya mtu na jambo; na kuna upendo wa ‘philadelphia’, upendo wa wanachama wa mashirika ya siri ambapo mtu humpenda mwenzake kama ndugu yake wakati si ndugu yake. Heri upendo wa ‘agape’ kuliko upendo ajmaina.

Ajmaina maana yake ni ‘wote’. Hivyo heri upendo wa ‘agape’ kuliko upendo wa aina zote. Kuelewa tafsiri ya neno ‘upendo’ ni hatua ya kwanza ya muhimu katika kuelewa tafsiri ya neno ‘Upendo wa Agape’.

Upendo ni neno maarufu la Kigiriki liitwalo ‘agape’ au upendo ambao watu wanao kwa sababu Mungu ameamua kwa hiari yake kuwapa kutokana na utiifu na unyenyekevu walionao kwake, na kutokana na kujitolea kwa ajili ya binadamu wenzao kama vile Yesu alivyojitolea maisha yake kwa ajili yetu. Watu ambao upendo wao wa ‘agape’ unafifia lazima Mungu aliwahi kuwapa upendo huo na wakashindwa kutimiza masharti yake, hivyo uhusiano wao na Mungu nao ukaanza kufifia.

Kuna watu wana talanta za kukaribisha watu na kuwafanya wajisikie wako nyumbani. Wanajua jinsi ya kujenga mahusiano mema, kunyenyekea na kuwatia watu moyo kwa kutumia ndimi zao. Hawa ndiyo aina ya leo ya mtume Barnaba, ambaye jina lake linamaanisha ‘mwana wa tumaini’ au ‘mwana wa faraja’. Hata hivyo, si kila mtu ana sehemu hiyo ya upendo wa Mungu kwa kiwango kikubwa; na kulikuwa na Barnaba mmoja tu miongoni mwa mitume wote. Ijapokuwa mitume wengine walikuwa na uwezo mkubwa pia wa kuhamasisha watu na kunyenyekea kwa njia zao wenyewe, ni mmoja tu aliyetajwa kwa kuwa na kipengele hicho cha upendo wa Mungu.

Wengine wanaweza wasiwe na kiasi cha kutosha cha upendo wa ‘agape’, lakini watatoa nguo zao kwa ajili ya maskini. Tena watazifua kwanza na kuzipiga pasi. Na kama kuna haja ya hizo nguo kuwa na ukubwa tofauti watahakikisha hilo pia linawezekana.

Mungu ni baba yetu wa kiroho. Hivyo basi, tunajua ya kuwa upendo wake umehifadhiwa ndani ya mioyo yetu. Kwa hiyo, kila mtu ana upendo wa ‘agape’ kwa kiasi fulani; lakini si upendo kamili. Upendo wa ‘agape’ kati ya binadamu na binadamu unahusiana na upendo wa kujitolea kwa ajili ya binadamu wengine. Kila mtu ana kiasi fulani cha upendo huo. Mtu akitaka awe na upendo kamili wa ‘agape’ sharti awe mtiifu na mnyenyekevu mbele za Mungu, na mbele ya binadamu wenzake, sharti ampende Mungu, na sharti ampende jirani yake kama anavyoipenda nafsi yake mwenyewe.

1 comment:

Roho Yako

289. Roho yako inatoka wapi? Ya kwangu inatoka Tanzania. Kwa sababu amani na utulivu ndivyo vitu vya muhimu zaidi katika maisha yangu. ...